Thursday, November 25, 2010

umeshawahi kutamani kurudi nyumbani?










Na Hafidh Kido

Dunia imefanya maonevu makubwa kwa wanadamu kufarakana na jamaa zao, kwasababu ya kuhangaikia maisha mepesi kuishi. Kila mtu ameshughulika na upande wake kiasi hadiriki hata kumtembelea jamaa wa karibu, japo kumjulia hali katika kitanda chake cha ugonjwa.

Namna hii polepole bila kujitambua tunazitenga tamaduni zetu na kukumbatia matamanio ya dunia; tunasahau tulipotoka na kujinasibisha na tulipo sasa, mradi tunapata tonge siku zinasonga. Dhuluma iliyoje kwa nafsi zetu wanaadamu, dharau isiyomithilika kurudi chini ya mchanga mikono mitupu; tazama jamii iliyokukuza imekutenga na Mola mwingi wa usamehevu pia amekukasirikia, kwasababu tu Dunia ilikutia upofu ukakumbatia hadaa zake.

Wengi tupo mbali ya ardhi tulizozikia vitovu vyetu; namaanisha bara, nchi, mikoa na wilaya tulizozawa na mama zetu, badala yake tupo mbali huko tukihangaikia maisha mepesi ama kazi nzuri. Lakini tunasahau kuwa kazi ama mshahara mzuri kwa mwanaadamu ni kutimiza malengo yaliyokufanya uje duniani.

Haina maana kujitesa na kujidhuru mwili kwa kukaa nchi za baridi ama joto kali, ukaacha kwenu kuliko na upepo mwanana na miti mingi itoayo harufu tamu ya utomvu wa matunda machanga ama maua ya kuburudisha mboni za macho na pua;  badala yake kujifutika mahala ambapo kuna msongamano wa magari, watu na majumba yaso mpangilio wa ramani.

Karaha ya moshi wa magari na kelele za viwanda zote hizo huzibua masikio yaliyozoea milio laini ya ndege waimbao kwa sauti za kupokezana. Lakini tunavumilia kukaa mahali pasipokubaliana na afya zetu, kwa maana Mola ni mwingi wa hekima kwa kuwaumba kila watu na hali zao za hewa.
Lakini tunadiriki kukaa sehemu ambazo hazikubaliani na maumbile yetu na wakati huohuo hatufuati kilichotupeleka huko. Tunaanza kusahau nyumbani na tamaduni zetu zilizotulea, tunatumia hovyo tunachokipata bila kukumbuka wazazi na ndugu tuliowaacha nyumbani kwa hadaa tu za kipato. Haipendezi katu.

Kama hiyo haitoshi tunabadili maisha yetu na kujinasibisha na uzungu, uhindi ama uarabu kulingana na bara tulilokuwapo, tamaduni zetu za upole, kusaidiana na kuoneana huruma zinapotea kama theluji katika mahali wazi; inanikera sana.

Haivutii hata kidogo kuona mtanzania anakaa ulaya miongo mitatu, hafikirii hata kurudi nyumbani na kufanya maendeleo. Mbaya zaidi hata watoto atakaowazaa hataki kuwapa majina ya nyumbani, hawazungumzishi lugha ya nyumbani wala hafikirii kuwatembeza mahali alipozaliwa hata siku moja.

Hata  fikira ndogo ya kibinaadamu ambayo haihitaji usomi wa chuo kikuu ni kuwa, tumekimbia maisha mabaya nyumbani na sasa tumeshayapata, je umewahi kufikiria kuisaidia jamii yako nao waondokane na dhiki uliyoikimbia? Ama unataka nao wakimbie kama wewe na jamii yenu ifutike kama zamani.. hapana hilo haliwezekani, ni upuuzi usiomithilika.

Katika historia nchi ya Australia na Marekani kuna watu ambao asili zao ni nchi hizo, lakini leo hii zinakaliwa na wazungu na watu wamesahau kabisa uwepo wa waanzilishi wa nchi hizo. Mfano Aboriginal ni watu weusi na ndiwo wenye nchi ya Australia, ila ukoloni umeshtadi katika nchi hiyo ukatafua uwepo wa watu hao ‘waaboriginal,’  mpaka sasa wamepotea; inaonekana  hawakua na mapenzi kwa nchi yao hata kutominyana kubaki nchini mwao. Tazama leo msomaji unashituka kusikia jina la Aboriginal kama watu wenyeji wa Australia,  wamepotea kabisa na kubaki katika vitabu vya kumbukumbu na majumba ya historia.

Kadhalika nchi ya Marekani wenyewe ni wahindi wekundu, lakini Christopher Columbus, ameigeuza historia ya watu hao na sasa imebaki kwenye vitabu na majumba ya historia tu kuwa wahindi wekundu ndiwo wenye Marekani. Na hii ni sababu ya kukosa uzalendo na asili zetu.  

Mwandishi anajaribu kucheza na maneno ili wanaadamu wajenge utamaduni wa kuthamini tamaduni zao na kukumbuka walipotoka. 

Inasemwa kuwa mtu asie na historia ni mtumwa,  hathaminiki. Leo hii wahindi wekundu wamekimbilia msitu wa Amazon, lakini wazungu wamefanya kila jitihada za kuwatumia kama nembo ya Marekani ila haisaidii kitu;  kwani walishaamua kuitupa nchi yao na kuwaachia wazungu, hivyo itabaki tu katika vitabu vya historia kuwa wahindi wekundu ndiwo wakazi halali wa Marekani lakini kimantiki haipo tena akilini.

Hushangai mji kama Dar es salaam, wenyeji wamekua ni wachaga, wadigo, wahaya na makabila mengine toka bara. Uroho wa fedha na kutothamini nyumbani kumefanya wakaazi halisi wa Dar es salaam kukimbilia mbali au kuhama mji kabisa. Haivutii..

Tazama ugomvi wa Palestina na Israel, waisrael walikuapo katika ardhi ile kwa miaka ya nyuma kabisa ila wakahama. Walikimbilia ulaya kutafuta maisha rahisi.

Nao  baada ya kufurumushwa na Adolf Hitler wa Ujerumani, waliamua kurudu kwao ila hawakua na pa kufikizia, ndipo walipoamua kununua ardhi kutoka kwa waarabu wa palestina.

Kilichotokea ni waarabu nao kufanya kosa lile lile walilofanya waisrael kwa kuthamini fedha kuliko ardhi na utamaduni wao, waliwauzia kwa fujo  bila kujua ardhi husogea upande wa waisrael kama maji yanavyokupwa na kujaa baharini; wamekumbuka shuka kumekucha wanaanza kuwafukuza katika mpaka wa Gaza wakidai wanaingiliwa katika mipaka bila kujua walikua wakiuza miliki yao kwa tamaa ya fedha. Sasa wanajuta. 

Ni vema kuanza kujithamini ukupenda ulipotoka ndipo watu wako wa karibu wataanza kukuthamini na kukuheshimu. kwa  maana heshima ya mtu huanzia kwake.

Anza sasa kutembelea kijiji ulichozaliwa na kama upo nchi za mbali jaribu kuweka katika ratiba zako  uende kwenu ukasalimie, kama umebahatika kupata mke na watoto usione haya kumuonyesha mkeo mahali ulipozaliwa hata kuwe kubaya namna gani.

Hivi huoni ngowa kupata kumbukumbu ya harufu ya maembe mabichi ulizokua ukipopoa na wenzio wakati mkirejea toka shule? Huoni ni fahari kumuonyesha mkeo, mumeo ama watoto wako kuwa mto huu ndiwo nilikua nikivuka kuenda na kurudi shule, ama katika nyumba hii inayotaka kuanguka ndipo nilipozaliwa na kukua mpaka hivi nimekuoa ama nimeolewa na wewe tukazaa watoto hawa… hutamani?

Hebu jaribu kuliweka hilo akilini, nina hakika litakusaidia katika kulinda na kuheshimu utamaduni uliokukolea, kadhalika itakusaidia kujivua na utumwa ulionao. Najua kuna fundo limekukaa kwa muda mrefu namna utakavyorudi ulipozaliwa ila unazuiwa na maisha ya kigeni yanayokufanya uone haya kuujulisha umma kuwa hivi nilivyo chimbuko langu ni hapa. Jaribu kufuta mawazo hayo na uanze upya.  Ishi wewe na si watakavyo wao.

No comments:

Post a Comment