Sunday, November 28, 2010

mapenzi ni maonevu?

Na Hafidh Kido

Tumekuwa walalamishi wakubwa juu ya wapenzi wetu kutukosea adabu, tunalaumu kuwa ni wenye kutoka nje ya makubaliano. Mara nyingi sababu huwa ni sisi kutozingatia alama za nyakati na namna tulivyokutana na mwenzi wetu.

Kuzingatia mazingira mliyokutana na mwenzi wako ni jambo muhimu katika mahusiano na mustakabali wenu; lakini wanaadamu tumekuwa tukilalamika kuwa hali imekua mbaya sasa tofauti na zamani, hali zamani ndiyo iliyokuharibia sasa. Mapenzi hupangwa mustakabali wake siku ya kwanza tu mnapoanza mahusiano, kinachosubiriwa ni hatma na sababu ya kuachana ama kugombana.

Tumekuwa tukitembelea wataalamu wa saikolojia juu ya mafarakano yetu, lakini husemwa mapenzi hayana ufundi. Hivyo ni vema kutafuta ufumbuzi wewe na mwenzio ima kwa kuuliza waliokuzidi umri, elimu au unaweza kuvuka mipaka ukaenda kumuuliza mpenzi wa zamani wa mwenza wako, usione wivu wala haya. Maana unaweza kugundua hata yeye alimpata baada ya kumkuta akigombana na mtu mwingine aliekua mpenzi wake, labda ndiyo hulka yake.

Mfano: inawezekana siku ya kwanza kuonana nae alikua anagombana na mpezi wake wa zamani, hivyo ili kumtia uchungu na kumdhihirishia kuwa yeye akiona ni wa nini wenzake wanajiuliza watampata lini anaamua kuwa na mahusiano na wewe. Akifanikiwa kumtia uchungu mpenzi wake kwa kuwa nawe fahuwa, lakini akiona kuendelea kuwa nawe hakumshitui kitu bibi au bwana Yule jiandae kuachwa ama kuandamwa na magomvi.

Watafiti wa masuala ya mapenzi duniani wanasema asilimia kubwa ya wanandoa hawana furaha na ndoa zao, wengi wakikumbuka siku waliyokula kiapo cha kuishi kwa raha na shida, hutamani siku zirudi nyuma akatalie palepale kanisani ama msikitini.

Sababu zipo nyingi, wengi huishi katika ndoa kwa kuwa mwenza wake ni chaguo la mama ama jamaa zake. Wengine wanaamua kuendelea kuwa katika ndoa ngumu kwasababu  wameshazaa na watoto  ni wadogo, kuwaacha wachague kati ya baba na mama itakuwa ukiwa mkubwa kwa watoto. Na mengi kadha wa kadha ambayo yanafichwa na viwambaza vya nyumba.

Tunaishi katika dunia ya kila mtu kujiamulia mambo yake, tofauti na zamani baba ndie muamuzi wa masuala ya nyumbani. Hivyo inakuwa ngumu kwa wanandoa kusikizana ama kuwa na nidhamu, kwa maana mafahali wawili hawakai zizi moja.

Tatizo ni nani awe myonge kwa mwenzie, mke anataka kudhihirisha kuwa sauti yake lazima iheshimike, na mume ana yale mazoea aliyorithi kwa mababu zake kuwa mume ndie mwenye sauti ya mwisho. Balaa ndipo linapoanzia hapo; na mbaya zaidi kila mmoja anafanya kazi na kuingiza kipato katika familia hakuna wa kumnyanyasa mwenzie kwa hali yoyote.

Elimu, nyote mmesoma na tena labda chuo kimoja na mkahitimu siku moja maana ndiyo mambo ya sasa hayo. Pesa, nyote mnafanya kazi na mna noti kichele za pesa katika kanzi au wazungu wanaita bank. Umri, mara nyingine mke ndie amekupita, tofauti na zamani mke lazima awe mdogo kwa mume ili apate kumuheshimu.

Hayo yote yanafanya ndoa za sasa kukosa nidhamu na umri huwa mchache kwa magombano ya kila siku. Adabu katika nyumba ikikosekana hata mapenzi hupungua. Hakuna uchawi mzuri katika mapenzi kama kusikilizana, kubali kuwa mjinga ila hakikisha msimamo wako unaeleweka.

Zamani wazee wetu walikua wakigombana na wake zao waliwatuma kijijini wakasalimu wazee,  mantiki yake ilikua ni kumlani shetani. Na mke akisharudi ana hamu na mumewe husahau yote yaliyopita. Ila kwa sasa huwezi kumtuma mke kijijini akakae tu, kwa hali ya maisha ilivyobadilika Watu wanafanya kazi sasa mke na mume, utamtuma kijijini na kazi amuachie nani?

Nilichotaka kueleza hapa ni namna ya wake zetu tunavyoonana nao katika siku za awali za mapenzi yetu, mfano mkeo umeanza kuonana nae katika kilabu cha pombe, ama ulimkuta nusu uchi ndipo ukapenda mwili wake kwanza; hivyo hali itakapobadilika na kurudi kama zamani ulivyomkuta usishangae.

Hivi utajisikiaje unamkanya mkeo asinywe pombe na amrudie Mungu au unamshauri asitiri mwili wake kwa kuvaa hijab au buibui, na anakujibu ‘kwani wewe uliponiona kwa mara ya kwanza nilikua msikitini au ulinikuta na buibui?’ eeeennnhhh!!? Utajisikiaje? 

Tafakari, chukua hatua kijana wa kike na kiume. Usikubali kuvutwa na matamanio ya nafsi yako, bali isikilize sauti ya Mungu anavyoshauri namna ya kumpata mume au mke bora. Naomba kuwasilisha.
 

No comments:

Post a Comment