Saturday, December 11, 2010

Hatuna ujanja lazima tule. Umelizingatia hili?



Na Hafidh Kido

Wanaadamu tumekuwa na viburi vingi kutokana na neema alizotujaalia muumba ardhi na mbingu, bila ya fahamu kuwa viburi hivyo huturudia wenywe pale tufikapo kikomo.

Hatujui tulitendalo! linaweza kuwa jibu la haraka kwa wale wavivu wa kufikiri. Lakini nakataa kuwa ni hivyo, kwa maana viburi tuvifanyavyo huazimia kabisa na mara nyingine tunatenda mchana kweupeee!!

Leo nimeamua kutoa mfano mdogo kabisa juu ya uwezo wa Mungu na udhaifu wa mwanaadamu. Kula: Naam hatuna ujanja katika hilo, juu ya viburi vyetu vyote na haraka ya kuhangaikia maisha lakini lazima tutafute kula. 

Husemwa njaa haina mjanja wala mwamba. Lakini tumejifunza nini katika tukio hilo ambalo tunaonekana kulizoea tu kuwa lazima tule; umepata kujiuliza halafu ya kula ni nini, kulala? Ama kuzidisha maasi kwa Mungu aliekujaalia baraka ya kupata kula.

Tazama, unaweza kuwepo katika shughuli iwe harusi au msiba, lazima katika ratiba kutakuwepo muda wa kula. Hudhani wanaadamu ni dhaifu kwa alietuumba na ndiyo maana hatuwezi kujizuia kula? Mpaka sasa umechukua uamuzi gani kumshukuru muumba wako kwa kukujaalia neema hiyo ya kupata kula.

Kwa maana nusu ya maisha yetu tunayatumia kutafuta kula. Madhambi mengi yanasababishwa na harakati za kutafuta kula. Magomvi na usaliti husababishwa na harakati ya kutafuta tonge. Umepata kutenga muda na kufikiri kuhusu hili?

Tumeamrishwa na dini kufanya ibada, lakini ibada yenye utulivu ni ile ifanywayo na kiumbe alieshiba, kwa maana huaminika katika dini kuwa kiumbe alieshiba ana utulivu wa nafsi. Mungu anasema ‘kuleni na kunyweni kisha mumuabudu aliewaumba.’

Hudhani kula pia ni ibada. Lakini tunakula kwa ibada kweli? Mimi na wewe tunapaswa kulijibu swali hili kwa mifano ya maisha halisi tunayoishi. Je tunakula ili tuishi ama tunaishi ili tule.

Dini iliyo na ukamilifu ya kiislamu inasema, mja anapokula hapaswi kushiba sana bali kiwiliwili chake kinapaswa kipate nguvu tu. Kwani kushiba sana huleta uvivu na maradhi; na pia haifai kulakula kila wakati kwani nako huleta maradhi na uvivu. Umelizingatia hilo?

Nchi zilizoendelea sasa zinapigana na ulafi usio na msingi, maana wananchi wake wamevimbiana na miili kupata maradhi ya mara kwa mara. Sukari, moyo, cholesterol, shinikizo la damu na saratani yamekuwa ni maradhi yaletwayo na kula hovyo. Umelizingatia hili?

Hatuwezi kuepuka kula, hata tuwe na nguvu kiasi gani. Hapa pana hekima kubwa sana na mazingatio kwa wenye akili. Umelizingatia hili?
 

No comments:

Post a Comment